Sunday, January 20, 2013

TAARIFA YA UTEKELEZAJI WA ILANI CCM KWA KATA YA KITANZINI MIYOMBONI JIMBO LA IRINGA MJINI


 Mheshimiwa  Jesca Msambatavangu  akifurahia  siku ya kampeni  zake za kuomba udiwani
 Hapa Jesca Msambatavangu (kushoto) akitekeleza ahadi zake kwa kikundi cha wajasiriamali.

Diwani  wa kata ya Miyomboni  Kitanzini jimbo la Iringa mjini Bi Jesca Msambatavangu
Ndugu wananchi katika uchaguzi wa mfumo wa vyama vingi vya siasa ili kushika Dola na kuunda Serikali kila Chama huandaa Ilani yake ya Uchaguzi.
 Ilani hutafsiri na kuelezea Sera zake na kuhusu maeneo muhimu ya siasa, Uchumi na jamii, na hutoa maelezo fasaha kuhusu mikakati ya utekelezaji wa sera zinazonadiwa pindi wagombea wake wakifanikiwa kushinda. 
Hivyo basi Chama cha Mapinduzi kilishinda na kushika Dola hivyo ilani yake ndiyo inayotekelezwa kwa kipindi cha mwaka 2010 hadi 2015.
Mimi pia ni mmoja kati ya wagombea wa CCM kwa ngazi ya kata yaani Diwani, katika kata ya Miyomboni Kitanzini ambaye nina wajibu wa kutekeleza ilani hiyo katika ngazi ya Kata hatimaye jimbo kwa kuungana na madiwani wengine katika manispaa yetu.
 Ifuatayo ni taarifa ya utekezaji wa Ilani ya CCM kwa kipindi cha mwaka 2010/2012 kwa ngazi ya kata ikiungana na jimbo.
SURA YA KWANZA
MAFANIKIO YA KIUCHUMI NA KIJAMII MIAKA 5 YA SERIKALI YA AWAMU YA NNE
Katika sura hii inaelezea utekelezaji wa Ilani ya uchaguzi ya Serikali ya awamu ya Nne kipindi cha miaka 5 (2005-2010). Ili lenga katika kutekeleza kipindi cha pili na cha mwisho cha mwelekeo wa sera za CCM katika miaka ya 2000-2010. Kwa kuzingatia Dira ya maendeleo ya Taifa ya 2025 na malengo ya millennia.
Inaelezea mafanikio yaliyopatikana, kiuchumi, kijamii na kisiasa.
SURA YA PILI
KUJENGA MSINGI WA UCHUMI WA KISASA WA TAIFA LINALOJITEGEMEA
Mwelekeo wa sera za CCM katika miaka 2010-2020 umeanisha jukumu kubwa la Nchi yetu; katika kipindi hiki ni kutekeleza lengo la dira ya maendeleo ya Taifa 2025 (Tanzania development vision). Ambalo Lengo ni;
 “Kuleta Mapinduzi ya Uchumi ulio nyuma na tegemezi na kuingiza katika mkondo wa uchumi wa kisasa wa Taifa linalojitegemea”
Ili kutekeleza dira hii ndiyo maana mwelekeo wa CCM kupitia Ilani; unaiagiza Serikali kutekeleza majukumu kupitia Ilani yake ambayo yatalenga kutimiza malengo ya millennia na Dira ya maendeleo ya Taifa. Ikiwa ni pamoja na kujenga Uchumi wa kisasa wa Taifa linalojitegemea yaani modernation ya Uchumi. Kwa kila ngazi, sasa wote pia kwa pamoja kuanzia ngazi ya mtaa hadi Taifa lazima tutekeleze malengo haya ya dira ya maendeleo kwa Taifa letu kila mtu kwa nafasi yake.
KILIMO
Kwahiyo kila sekta kama ni Kilimo wajue lengo ni kujenga Uchumi wa kisasa  utakaopelekea  Taifa letu kujitegemea. Wadau ambao ni wakulima, maafisa ugani au kilimo, wazalishaji wa pembejeo kama mbolea na mbegu, wauzaji wa pembejeo, vyuo vya mafunzo ya kilimo wote kwa pamoja wajue tunajenga uchumi wa kisasa utakaopelekea Taifa letu kujitegemea. 
Sasa kama wengine wanazalisha mbegu bora, wauzaji wanachakachuka, wakulima wanapewa mbegu na mbolea za ruzuku wanauza vocha, Vyuoni hakuna utafiti wakutosha kusaidia mapinduzi haya ya kilimo ni tatizo katika kufikia mpango wa maendeleo wa Taifa letu; ambalo tunategemea sisi na watoto wetu waendelee kuishi humu.
Sasa basi Ilani hii 2010-2015 inalengo la Kuongeza KASI ya ujenzi wa Uchumi wa Kisasa na Taifa linalojitegemea kwa kuwashirikisha na kuwawezesha kiuchumi wananchi.
Kwa vipi?
Kuongeza maarifa na matumizi ya sayansi na Teknolojia katika sekta za Uzalishaji. Ili kuongeza Uzalishaji,Ufanisi na Tija au faida katika uchumi hususani katika:
·     Kilimo 3(31-56) -ndipo ikaanzishwa program ya Kilimo kwanza.  Ambayo itaelezea upatikanaji wa Fedha za uwekezaji katika sekta ya Kilimo; Mbegu bora; Zana za kisasa; Matumizi ya mbolea; Elimu kwa wakulima kuhusu kanuni za kilimo; huduma za ugani; mikopo kwa wakulima; upatikanaji wa masoko; utafiti na matokeo; kuongeza thamani ya mazao ya kilimo.   
·     Ufugaji – Kubadili wakulima kutoka ufugani duni na kuwa wafugaji bora, sio tu wakuhama hama. 
Kutatua matatizo ya  malisho na maji kuwafikisha wafugaji katika ukulima mchanganyiko na ufugaji wa mabandani, wenye tija kubwa utakao toa nyama na maziwa bora. 
Ili kujenga uchumi wa kisasa na kujitegemea. Ndiyo maana mjini kuna Nyama na maziwa.
 Bila mipango hii wale watoto wetu vichanga wangekunywa nini; hizo nyama choma zingekuwepo.
·     Uvuvi – Mkazo unalenga katika kuwapatia wavuvi maarifa yatakayobadili na kuongeza uzalishaji wa samaki. 
Samaki wakiongezeka wanaonufaika sio wavuvi peke yao kwa kupata faida; lakini pia wauzaji wa samaki na walaji wa samaki. 
Mwisho uchumi utaimarika na watu kujitegemea.
 Pia Serikali katika hili, inatilia mkazo uwezeshaji kwa wavuvi, kuendeleza viwanda vya samaki, na kusimamia uvunaji endelevu wa samaki.
·     Viwanda – Kutoa msukumo katika mapinduzi ya viwanda; kuhamasisha maendeleo ya Sayansi, teknolojia, na uhandisi, viwanda vya msingi, kati na vidogo. Ikiwa ni pamoja na kusimamia viwanda ambavyo tunavyo vya watu binafsi na Serikali.
NB:Mikakati mbali mbali inatekelezwa kama; MKURABITA, Ushirika, Mfuko wa Pembejeo za Kilimo, Mifuko ya uwezeshaji,Mfuko wa maendeleo ya Jamii na Benki ya wanawake.
SURA YA TATU
SEKTA YA UZALISHAJI MALI
KILIMO-3(31-38)
UTANGULIZI
Ndugu wananchi watu wengine wanabeza swala la kilimo kwanza. Hivi kweli chakula sio kitu cha kwanza katika Nchi? Unaweza ukafanya cho chote unachofanya kama haujala?  Swali huwa linaulizwa; UNAISHI ILI ULE AU UNAKULA ILI UISHI? JIBU 1.UNAKULA ili UISHI ndiyo jibu sahihi. 2.Wale wanaobeza Kilimo kwanza ndiyo ambao wangejibu UNAISHI ili ULE.
Sasa kama watu wote sisi milioni 44 na kitu lazima tule hata kama ni mlo mmoja kwa siku, nadhani kilimo ni kwanza.Kuvaa unaweza ukavaa nguo mbili kwa wiki lakini hauwezi kula ugali ule ambao ulisha kula jana ukatoka tumboni ukala leo.
 Hiyo ndiyo maana kilimo lazima kipewe kipaumbele.
Hata kulala utalala kitanda na nyumba hiyo hiyo kwa miaka mingi lakini sio kula.Na hapo na ufugaji uko ndani yake. 
Na kama kilimo hakitiliwi mkazo inakuwaje ninyi hapa sokoni kila siku wengine tangu wazazi wenu, tangu utoto mpaka mnazeeka mnauza tu malimbichi zinatoka wapi?
PEMBEJEO ZA KILIMO-3(32d)
Mbolea za ruzuku na mbegu bora; zimetolewa na hasa ilikuwa kuwasaidia wale watu wasio na uwezo kabisa, sio kuwatosheleza kuwasaidia. Kata yetu sisi kutokana na mazingira yake mbolea hizi tumepewa vocha 59 vipaumbele tuliwapa vijiji zaidi. Na zimetolewa kwenye mitaa yetu yote.
Tatizo pia ni uelewa kwamba wapewe wale wasio na uwezo, lakini pia wengine wanapewa vocha wanaziuza, shambani hatumii tena, wala shamba hana. 
Lakini pia kuna mbolea za samadi na mboji watu wanaweza kutumia pia.
Uanzishaji wa uzalishaji wa mbegu bora kupitia majeshi lakini pia, kutoa ruzuku kwenye dawa za mifugo nk.
Sisi kama Kata ya Miyomboni Kitanzini tunanifaika na kilimo kwanza hasa kwa sababu tuna masoko yote makubwa hapa, ambayo huuza bidhaa za mashambani, hivyo kutuimarishia uchumi wetu.
UVUVI-3(39)
Kata yetu inanufaika na sera hiyo kwani zaidi ya kupata kitowe cha Samaki lakini kiuchumi ni biashara yetu. Kwa kweli tunaonga mipango endelevu kwa uhai wa samaki ili tuendelee kufanya biashara ya samaki.
UTALII-3(45)
Utalii unaendelea kukua katika mji wetu, hata sisi tumeona faida za moja kwa moja za utalii. Mfano hapa sokoni, soko hili la zamani ni la kihistoria na lilikuwa soko la kwanza Africa. Ndiyo maana wazungu wanakuja kuja kula humo ndani kwa akina mama. Akina mama inabidi mjitahidi yes na no zisiwapige chenga.
Ila nadhani kuna changamoto ya mlango na maji kutiririka sehemu Fulani na dhani kina mama waseme vizuri ili tuone namna ya kuboresha.
Lakini sisi kata yetu ina hivyo vitu viwili vya kihistoria kama vivutio vya utalii, ambalo hili soko na Eneo la Kitanzini ambapo walikuwa wananyongewa watu. Na manispaa imeshaanda mpango wa kupaendeleza ili kutunza kumbu kumbu hiyo, pamoja na vingine vilivyo ndani ya manispaa.
SURA YA NNE
ARDHI-4(57-59)
Ardhi ni raslimali muhimu katika kuchangia maendeleo. Ina umuhimu kabla na hata baada yakuendelezwa ili mradi tu ikithaminishwa na kutambulika kisheria uthamani wake.
Upimaji wa Viwanja/maeneo 4(60c)
Manispaa kupitia sisi madiwani wake na watendaji, tuliliona hili kuwa ni hitaji kubwa kwa wakazi wetu kwa ujumla, hasa makazi. Hivyo tulipendekeza ili kuendana na kasi yakukua kwa uhitaji wa viwanja kunakotokana na kukua kwa uchumi; ni vyema tukanunua vifaa bora kwaajili ya upimaji. Hivyo manispaa yetu sasa ina vifaa vya kisasa vya upimaji ambavyo kwa Manispaa zote Tanzania ni Manispaa mbili tu yenye navyo yaani Arusha na Iringa. Vyenye uwezo wakupima viwanja 100 kwa siku. Viwanja 400 na zaidi vilipimwa na kugawiwa eneo la ngelewala, 100 eneo la mafifi, na maeneo mengine yanaendelea kupimwa.
Changamoto tulio nayo ni kutokuwa na ardhi yetu wenyewe. Ardhi inayopimwa tunaichukua kwa wananchi kwa kulipa fidia, kisha kupima kuwa uuzia au kuwagawia watu tena. Fidia pia kwa kadri mji ulivyoendelea inakuwa kubwa kidogo.
Utaratibu wa ugawaji pia umeboreshwa. Kwamba kila fomu inayotolewa maanake ni kiwanja. Sasa tulichogundua tena wanao kuja kuchukua fomu zile wengine wanajihimu saa 10.00 usiku, sio wa hitaji wa viwanja wanakuwa tena madalali.
 Kwahiyo kachukua fomu kwa 10,000/= anaiuza 50,000/= mpaka 200,000/=. Sasa hii tena ni shida, cha msingi tunawaomba wananchi muwe mnasoma matangazo yetu, au kusikiliza matangazo, maana hata kiwanja pia unaweza ukalanguliwa.
Kuna njia nyingine ambayo mnaweza kupiwa viwanja, kwa kuomba ofisi za ardhi manispaa ziwapimie kwa kuchingia gharama kwa pamoja. Ila sharti mtatakiwa mruhusu miundo mbinu yote kupita kwenye maeneo hayo, kama bara bara nk.
MIPANGO MIJI-4(60b)
Sheria za mipango miji zimeendelea kufuatiliwa, kuzuia ujenzi holela kati kati ya mji. Natunawaomba wananchi waendelee kufuata sheria za mipango miji ili kuruhusu kada nyingine kufanya kazi pia bila bughudha.
MKURABITA
Huu ni mpango wa Serikali ya CCM ambao ni mkakati wa Kurasimisha raslimali na Biashara Tanzania. 
Kwa lengo la kutambua rasmi au kisheria raslimali za wanyonge ambazo bado ziko kwenye sekta isiyo rasmi, ili zitumike kuwawezesha washiriki kwenye uchumi rasmi wa Taifa. Yaani kutambua nyumba ambazo zimejengwa katika maeneo yanayoruhusiwa kisheria na taratibu, lakini hazina hati milki. 
Ziweze kukatiwa hati milki ili watu hawa wawe kutumia nyumba hizo kama corallater au dhamana za kupatia mikopo katika taasisi mbali mbali za fedha na kuboresha, kuinua au kuanzisha shughuli ya kumuinua mtu kiuchumi na kisha kujitegemea.
 Kwa manispaa yetu ya Iringa chini ya usimamizi wa madiwani na kwa kushirikiana na watendaji pia, kazi hii itaanzia Kata za Mwangata, kisha hata Kitanzini tutanufaika na mpango huu wa MKURABITA.
MAJENGO/NYUMBA-4(60a)
Ujenzi na aina ya nyumba zinazojengwa pia ni ishara ya maendeleo ya kiuchumi ambayo pia huchochea uchumi kuendelea kukua. Nyumba nyingi zimeboreshwa baada ya manispaa kutunga sheria ya kufungua vichochoro. Hii imetoa fursa kwa nyumba nyingi kufungua milango ya maduka mengi ambayo yameinua kipato kwa wenye nyumba na wapangaji pia. Vibali pia vilitolewa kwa wenye nyumba kukarabati nyumba zao. Na wengine wamepata fursa ya kujenga maghorofa yameongezeka, hali inayoashiria kukua kwa uchumi.
NISHATI-4(61)
Moja ya matatizo makubwa yaliyikuwa yanavikumba viwanda vyetu pia, hadi vikapelekea vingi vyake kuzaliza hasara ili kuwa ni upungufu wa nishati ya umeme. Ikiwa ni pamoja na matatizo ya menejimenti. Hivyo naamini mwaka huu mgao wa umeme umepungua sana, na kwa mikakati ya mbele pamoja na upatikanaji wa gesi naamini itatusaidia kutekereza vyema sera ya mapinduzi ya viwanda.
SURA YA TANO
UWEZESHAJI WANANCHI KIUCHUMI
Lakini ili wananchi ili waweze kumiliki uchumi lazima wawe na maarifa ya kisasa. 5(76a) Ilani inasema kufufua kwa nguvu zote elimu yenye manufaa ya watu wazima nchini kote ili masomo ya ujasiriamali,uwezeshaji, urasmishaji wa biashara, kilimo, ufugaji na uvuvi yawezekutolewa kwa wananchi wengi; Hatua za kutoa mafunzo ya ujasirimali lazima zichukuliwe;
Ndugu wananchi ili watu waweze kujenga uchumi wa kujitegemea, hususani wananchi wa Kata ya miyomboni kitanzini. 
Ambayo kwa kiasi kikubwa imesheheni wafanyabiashara wakubwa na wadogo.
 Wanahitaji kupata maarifa hasa ya Elimu ya ujasiriamali ili kufanya biashara zao kwa ufanisi mkubwa.
Ndugu wananchi, mimi baada yakuliona hilo niliona umuhimu wakupata mafunzo hayo ya ujasiriamali. Ambayo yalifanyika mara mbili katika ukumbi wa warfare na Saba Saba CCM. Ambayo yalihusisha 1.utengenezaji wa bidhaa mbali mbali za viwandani kama utengenezaji wa sabuni za miche, sabuni za maji, dawa zakuoshea au kudekia, dawa za vyooni nk. 2.Usindikaji wa vyakula mbali mbali. 3.Mafunzo ya ufugaji bora wa mifugo mbali mbali kama kuku na utengenezaji wa chakula chake, Ng’ombe, mbuzi nk
USHIRIKA-5(76b)
Jumla ya makundi 18 ya watu hamsini hadi sitini yawajasiriamali yalianzishwa ambao jumla yao ni zaidi ya 1080. Na ofisi yangu ya Diwani iliwasaidia kuandika katiba na kusajiliwa rasmi manispaa. Vikundi hivyo ni Mshikamano, Saba saba no.1, 2,3; Nuru Group, Ebenezer Group, Tuwezeshe, Amani, Nams Group, Juhudi Group nk Pia makundi ya vicoba ambapo katika Soko la Mashine tatu pekee yake kuna vicoba vitatu. Idadi ya vikundi vilivyoundwa katika Kata viko zaidi ya 20 na 15 vimesajiriwa tayari na 5 vinaendelea na mchakato wa usajiri. Hivyo jumla ya vikundi vyote 38.
Wajasiriamali pia walielezwa fursa zilizopo zakukopa katika Taasisi za kifedha zilizopo ndani ya Kata yetu na Nje kama mabenki kama NMB, na taasisi nyingine kama FINCA, Pride na SACCOS na VICOBA.
Pia walielezwa na kufundishwa namna yakujiwekea pesa au kusave kama njia mbadala ya kupata mtaji.
AJIRA NA UWEZESHAJI WANANCHI-5(77)
UBORESHAJI WA MASOKO
Hii pia ni njia mojawapo ya kujenga uchumi, kwani hutoa fursa kwa wafanyabiashara kuendelea kufanya kazi zao kwa ufanisi mkubwa. Kutokana na ongezeko kubwa la wafanyabiashara hasa katika kata hii, Manispaa kwa kushirikiana na wadau wa soko kuu wameboresha soko kuu kwa kushirikiana na wafanyabiashara. Lakini ili kupunguza msongamano masoko mawili yameongezwa katika kata hii. Ambalo ni magari mabovu na  mashine tatu ambalo bado mpango wakuliboresha zaidi, hasa wakati wa masika unaendelea. Kwani eneo hili linamilikiwa na wenzetu wa Bakwata pia.
Hata hivyo mimi kama Diwani nimeweza kushirikiana na wana mashine tatu kuhakikisha lile linalowezekana angalau kutunusuru mvua limefanyika kwa kutoa trubai la kuezekea eneo la matunda.
FURSA ZA KIBIASHARA VIJANA-5(78)
Ndani ya kata yangu vijana wengi wamenufaika na kuruhusiwa kwa biashara ya pick-pick alimaarufu boda boda, ambazo zimetoa ajira kwa vijana asilimia kubwa.
Pia kuna fursa ya Toyo, mikokoteni ambayo kwa kiasi kikubwa inatupa changamoto ya kuhakikisha bara bara zote zinatumika kwa matumizi yaliyokusudia ya vyombo vya usafiri.
VIJANA
Mafunzo ya ujasiriamali yalitolewa katika Chuo kikuu RUCO ambayo mimi mwenyewe niliyatoa kwa vijana wa timu za mbili za mpira wa miguu kutoka katika kila kata ambazo jumla zilkuwa timu 40 ukiongeza na za vijiji.
Pia mitaji ya mabero ya mitumba nane ili tolewa kwa vijana wa timu za mpira wa miguu mbili kutoka katika kata ya Miyomboni Kitanzini; ambazo ni Maghorofani FC  na mashine tatu FC. Pia gunia 10 za mahindi zilitolewa kama mtaji kwa vijana wa mpira wa miguu Ipogolo United. Na sabuni za kuogea zenye dhamani ya sh.700,000/= zilitolewa kwa timu ya mpira wa miguu wanawake Ipogolo. Bero kumi za mitumba zilitolewa kwa vijana wa Iringa Youth club; belo mbili zilitolewa kwa vijana wa kundi la maigizo kihesa- Umati; Jumla ya fedha taslimu milioni mbili zilitolewa kwa mabinti walioterekezwa na wazazi au watu waliowapa ujauzito; ambapo niliwaanzishia kibubu program. Baiskeli zilitolewa kwa watoto wa mitaani na mafunzo na mashine ya kujzia tyre upepo.nk
Wapiga debe, wasukuma mikokoteni, makuli, wauzaji wadogo wadogo;
Waliundiwa uongozi na kupewa vitambulisho na unifomu ili kufanya kazi zao kwa ufanisi. Lakini pia walipewa elimu ya kuepukana na tabia zinazowafanya wadharaulike katika jamii kama;
·     Wizi
·     Ulevi uliokithiri
·     Lugha za matusi
·     Uchafu
Waheshimu kazi yao na kuwa raia wema na pia washirikiane na polisi kwa ulinzi shirikishi katika maeneo yao. Na mengine mengi yamefanya kwa vijana hata yaliyo nje na Ilani ya uchaguzi. Kama kuwasaidia kuwalipia ada za chuo. Kushirikianao katika sherehe zao kama mwaka mpya nk.
Kushiriki kuzindua kanda au CD zao katika matamasha mbali mbali. Kuichangia timu ya polisi na mageraza.
Kutelembea wafungwa na kuwa misaada ya ya sabuni za kuogea 800 na limu za karatasi kumi. Kuchangia mikutano ya vijana wa CCM, Kuwasaidia hata wale vijana ambao sio wa upande wetu. Kuchangia uanzishaji wa vikundi wa vya kijasiriamali kama Ipogolo. Kushiriki katika shughuli za kijamii; kama misiba, harusi, sherehe za vyuo vikuu, makanisa, misikiti nk.
MIUNDO MBINU
MAWASILIANO na USAFIRISHAJI/UCHUKUZI
Ndugu wananchi katika kukuza uchumi, mawasiliano ni kitu cha muhimu, ambayo huwezeza mzunguko wa biashara au huduma kuwa rahisi. 2.(d). Mawasiliano ya simu za mkononi na hata za meza ndani ya kata yetu hakuna shida. Watu wanaagiza mizigo kwa simu wanatuma pesa kwa simu. Hivyo imesababisha kurahisiha ufanyaji wa biashara nakuongeza tija na maendeleo. Hata Kata yetu haitakuwa na matatizo yo yote kuhama kutoka analogy kwenda digitaly.
BARA BARA
Bara bara zimeimarishwa katika kata yetu na zinapitika kwa misimu yote kwaasili mia 99% kama sio 100%.
Mapungufu madogo yalipotokea mwaka jana wakati wa mvua kubwa basi, marekebisho yalifanyika hasa kwa bara bara ya mtaa wa mlimani. Bado tunachangamoto kwa Bara bara kubwa karibu na eneo la sigara ambalo mara nying mvua zikinyesha maji hufulika kwa kuwa karavati la eneo lile limetitia hivyo kushindwa kupitisha maji kwa wingi. Swala hili limefikishwa kwa mamlaka husika yaani Tanroads na wameahidi kulishughulikia wakati wa mchakato wa kutengeneza bara bara ya Iringa mpaka Dodoma.
Ununuzi wa Greda
Kwakuona pia mara nyingi bara bara zetu zinaharibika hasa wakati wa mvua kubwa kama mwaka jana. Nausumbufu unakuwa mkubwa, pia kwakuwa tulikuwa tunataka kila sehemu tunapopima viwanja angalau tutengeneze njia za mitaa inayoonyesha jinsi viwanja vilivyogawika.
Basi, tulipendekeza madiwani  ufanyike uchakato wakutafuta greda. Ambao ulianza kwa kurasmisha mali zetu za manispaa hasa majengo ambayo hayakuwa na hati, ili tupate dhamana yakutosha kuwekezea ili tuweze kukopesheka. Mchakato ukakamilika hatimaye, tukakopeshwa fedha na benki ya CRDB ambayo imetuwezesha kununua Greda.
SURA YA SITA
HUDUMA ZA JAMII- ELIMU
MSINGI – 6(85
Ndugu wananchi; ndani ya Kata yetu tuna shule ya sekondari Miyomboni na sule ya msingi ni Azimio.
Watoto wote wenye umri wa kujiunga na shule ya msingi yaani miaka saba wamepata nafasi ya kujiunga na shule ya msingi kwa…….asilimia
Ili kubaini matatizo yanayowapata watoto wa shule za msingi nilifanya nao mkutano. Walitoa kero zao na ziliwasilishwa kwa Mkuu wa Shule; ikiwa ni pamoja na kuomba walimu wasiuze, vitu darasani. Kwani huwa vinawapunguzia umakini katika kusoma wanapofundishwa, kwa kufikiri kitu kinachouzwa na kupopeshwa. Lakini pia huwasababishia kutoroka shule wakikopeshwa wakakosa hela ya kulipa; huogopa kwenda shule.
Watoto pia waliomba wazazi wao kuwa karibu nao nakupata muda wa kuwasikiliza wanapokuwa na shida. Hasa kuwapa chai yenye kitafunwa asubuhi. Akina baba pia wasiwaonee akina mama na akina shangazi.
Kero yao nyingine kubwa ni kutokuthaminiwa hasa kwa kutowatengea au kuendeleza maeneo ya michezo. Hivyo waliomba mipira na jezi. Timu mbili za watoto walipewa mipira na jezi, ambazo ni Kitanzini United Stars na Mshindo wanderous.
WALIMU
Pia walitoa mapendekezo na malalamiko yao huku wakiomba ushirikiano mkubwa kutoka kwa wazazi; ili kujenga malezi bora.
Wakitoa mfano wakukosa ushirikiano walisema ni pale walipobaini kuwa mtoto mmoja aliyekuwa akisumbua sana na mtoro wad rasa la sita alipowajibu amechelewa kwenda shule alikuwa kuwekwa vipandikizi vya kuzuia mimba. Na hii ilionyesha wazi kuwa mlezi alikuwa anajua.
 Pia walitoa malalamiko ya baadhi ya changamoto wanazokutana nazo kama wizi uliokithiri kwa maeneo ya shule, ukarabati wa shule kuwa muhimu, pia nilipata fursa ya kuchangia mahitaji ya shule hiyo. Pia tuliwaomba polisi kusaidia ulizi wa maeneo hayo. Usimamizi wa karibu zaidi upo chini ya kata ya mshindo.
SEKONDARI
Kuwa sekondari ya Kata, kuendelea kusimamia ufaulu wa kuhakikisha zaidi ya asilimia hamsini ya watoto au zaidia wanafaulu na kujiunga na kidato cha kwanza ifikapo mwaka 2015. Kiwango cha ufaulu kwa watoto wetu Miyomboni kimekuwa kikiongezeka kwa……….
UJENZI,
Ilani inatakakuendelea kuboresha shule kwa ujenzi wa maabara, madarasa, vyoo, nyumba za walimu, nakununuavifaa vya shule.

No comments:

Post a Comment